Mwenyekiti wa kamati ya ujenzi atakiwa kutema fedha alizokwapua

 

Mwenyekiti wa kamati ya ujenzi wa chumba cha darasa la shule ya msingi Ukombozi,kijijij cha Kiegei B,wilaya ya Nachingwea,Fanyeni Lipalapi ametakiwa kurejesha shilingi 533,000 ambazo alijipatia kinyume cha sheria katika ujenzi huo. 

Agizo hilo lilitolewa jana na ofisa katika ofisi ya mkuu wa wilaya ya Nchingwea,Jeremiah Mlwafu aliyemwakilisha mkuu wa wilaya hii wakati wa mkutano wa mrejesho wa ufuatiliaji wa matumizi ya raslimali za umma,uliofanyika jana katika mamlaka ya mji mdogo wa Nachingwea. 

Mlwafu ambae pia ni ofisa tarafa wa tarafa ya Nachingwea,alisema mwenyekiti huyo wa kamati ya ujenzi anatakiwa kurejesha kiasi hicho cha fedha kama alivyoagizwa na kamati ya maendeleo ya kata ya Kiegei.Iwapo hatatekeleza basi hatua kali dhidi yake itachukuliwa. 

Akionesha kukasirishwa na kitendo kilichofanywa na Lipalapi,alisema amelazimika kutoa agizo hilo kutokana na kuheshimu maamuzi ya kamati ya maendeleo ya kata.Kama yasingetolewa maamuzi hayo asingesita kuchukulia hatua za juu zaidi. 

Mbali na kumtaka mwenyekiti huyo wakamati kurejesha fedha.Lakini pia aliagiza ufanyike ufuatiliaji ilikujiridhisha na taarifa za upotevu wa shilingi 2.00 milioni za ujenzi wa vyumba vya madarasa ya shule ya sekondari ya Kilimarondo. 

"Hata hivyo sivizuii vyombo kufuatilia suala la mwenyekiti wa kamati ya shule ya Ukombozi.Bali ninachoagiza nikurejesha fedha hizo ambazo zingetumika kwa ujenzi,halafu yeye akazitumia kwa mambo yake binafsi,"alisema Mlwafu. 

Mlwafu licha ya kuzipongeza  kamati  za ufuatiliaji matumizi ya rasilimali za umma ( PETS)za kata aliziasa kamati hizo kuwa karibu na ofisi za tarafa.Kwani zinamuwakilisha mkuu wa wilaya kwenye eneo la utawala la tarafa.Hasa zinapoona baadhi ya mambo yanakosa utatuzi baada ya kupeleka kwenye mamlaka za chini ya tarafa. 

Awali kaimu ofisa mtendaji kata wa kata ya Kiegei,Mshamu Limbanga alisema kamati ya ufuatiliaji matumizi ya rasilimali za umma ya kata ya Kiegei iligundua ubadhirifu wafedha za ujenzi wa chumba cha darasa la shule ya msingi Ukombozi. 

Alisema jumla ya fedha zote ambazo zilipelekwa kwenye ujenzi wa chumba hicho ambazo zilitokana na ushuru wa mazao zilikuwa shilingi 833,000.Hata hivyo shilingi 300,000 zilitumika kununua saruji kwa ajili ya ujenzi huo.Kiasi cha fedha kilicho stahili kubaki(shilingi 533,000) ndicho kilichochukuliwa na Lipalapi. 

"Kamati ya maendeleo ya kata iliamuru tarehe 19,mwezi na mwaka ujao(19.1.2019) arejeshe fedha hizo.Kwakweli mradi unatekelezwa kwa ubabaishaji mkubwa.Mbali na fedha lakini tofali 720 ni mbovu,hazifai kujengea.Zimetengenezwa chini ya kiwango,"alisema Limbanga. 

Kamati za PETS za kata zinawajibika kwa shirika la msaada wa kisheria kwa wanawake na watoto wa Lindi(LIWOPAC) ambalo linatekeleza mradi wa ufuatiliaji matumizi ya Rasilimali za umma katika sekta ya elimu ya sekondari.Ambapo katika wilaya ya Nachingwea mradi huo unatekelezwa kwenye kata za Kiegei,Kilimarondo,Namapwia na Nditi.

No comments

Powered by Blogger.