Hamasa ya mafanikio juu ya watu wanaokuzunguka

Katika sayari hii ya wasakatonge imezungukwa na watu wengi sana, hivyo ili uweze kufurahia uwepo wako hapa duniani unatakiwa kufahamu namna  sahihi ya kuishi vyema na viumbe hao. 

Hii ni kwa sababu ni bora kuishi na simba kuliko kuishi na binadamu. Yupo pia msanii Fulani aliwahi kuimba katika wimbo wake akisema ni bora wali nyama kuliko walimwengu,  hii ni kwa sababu binadamu hawa ni viumbe wa ajabu sana. Wao ndio wanaongoza kuwa na visirani visivyokuwa na maana. 

Viumbe hao kazi yao kubwa ni kusifia midomoni huku moyoni wanabeza, kwa maneno mengine tunaweza kusema yaani  wao wapo katika  dunia ili kuona  wewe unazidi kuwa maskini kila kukicha. Hivyo ili uweze kuishi na kufurahia uwepo wako hapa duniani unatakiwa kufahamu namna sahihi ya kuishi kwa akili hasa unapokuwa katika dunia hii. 

Si kila kitu unachofanya ukafikiri kila mtu anakipenda, Watu wengi watasema mengi lakini haina maana kila kitu wanachokisema uchukue. Kimsingi maneno ya watu yapo ambayo yanajenga kwa namna moja ama nyingine, lakini   yapo  maneno mengine ambayo hayajengi kabisa. 

Hivyo akili yako ni lazima itulie ili iwaze kupambanua ni lipi jambo jema na ni lipi baya, kwa mfano kama  leo hii ukitaka kufanya biashara fulani pindi utakapokwenda kumshirikisha mtu ambaye yupo karibu yako ili kuomba ushauri, kwa kuwa  mtu huyo ana chuki zake binafsi juu ya maendeleo yako  atakwambia biashara hiyo haifai, mwishoe  kwa kuwa wewe mwenyewe hauna imani unajikuta unabadilisha mawazo na kufanya jambo jingine. 

Hivyo ndugu yangu, Sina maana ya kwamba eti kuomba ushauri kwa watu wengine  ni dhambi! Hapana, ila unatakiwa kuomba ushauri kwa watu sahaihi, pia ikumbukwe kuwa  maisha halisi juu yako unayo wewe mwenyewe, hivyo kwa kila kitu unachoshauriwa unatakiwa ukichuje vyema ili ujue kama kina mashiko kabla ya kuamua kuwashirikisha wakatishaji tamaa. 

Mwisho naomba nimalize kwa kusema  “si kila mfuko unafaa kuwekwa pesa”. 

No comments

Powered by Blogger.